Wazee mkoani Lindi wameomba kupewa kipaumbele katika maeneo yatolewayo huduma za kijamii ikiwemo hospitali na wametoa mapendekezo yao ili kuboresha huduma kwa wazee katika jamii ikiwa ni pamoja na kuundwa kwa sheria itakayotoa adhabu kwa vijana wanaokwepa jukumu la kuwatunza wazazi wake kipindi cha uzee.

Wazee waliohudhuria kikao cha Baraza la wazee wa Mkoa wa Lindi

Wameyazungumza hayo katika kikao cha kwanza cha kamati ya wazee mkoa wa Lindi kilichofanyika leo Februari 14, 2023 katika ukumbi wa mikutano ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Mganga Mkuu Mkoa wa Lindi, maafisa ustawi wa jamii, wajumbe kutoka timu ya uendeshaji wa huduma za afya mkoa (RHMT), wawakilishi kutoka vyama vya utetezi wa haki za binadamu na waandishi wa habari huku mgeni rasmi katika mkutano huo akiwa ni Dkt. Bora Haule (Phd) ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi - Viwanda, Biashara Na Uwekezaji ambaye amemuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Lindi Bi. Zainab Telack ambaye amewaomba wazee kuacha kupokea majukumu mazito katika umri wao ikiwemo kuwatunza wajukuu.

Dkt. Bora Haule (Phd) ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi - Viwanda, Biashara Na Uwekezaji
akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Wazee Mkoa wa Lindi

Baraza la wazee mkoa wa Lindi limeanzishwa mwaka 2022 likiwa na lengo la kuwalinda wazee na kuhakikisha wanapata usimamizi na msaada wa karibu ili kuleta ustawi wa jamii bora kwa kuwa hawana nguvu tena ya kuhangaika katika nyakati zao za uzee.

Naye Mganga mkuu wa Mkoa wa Lindi Dkt. Henry Kyaga ameipongeza serikali kwa hatua mbalimbali zilizofikiwa katika kuwalinda na kutambua nafasi ya wazee katika jamii licha ya ukweli kwamba, katika ngazi ya mkoa bado hawajafika katika kiwango cha ubora katika kuyatekeleza hayo. Hivyo ametoa wito kwa madiwani katika halmashauri zote kuyasimamia mabaraza haya ili yawe hai.

Aidha Dkt. Henry Kyaga ameahidi kuandaa mazingira mazuri kwa ajili ya kuwahudumia wazee ili kuepukana na changamoto wanazokutana nazo huku akishauri kuhakikisha vikao vya mabaraza ya wazee vinafanyika katika ngazi za vijiji, kata na wilaya kwani baadhi ya changamoto zinaweza kutatulika katika hatua hizo.

Post a Comment

Previous Post Next Post