Serikali imeendelea kutekeleza ahadi ya kupeleka umeme wa uhakika katika mikoa ya Lindi na Mtwara ambapo Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba ameongoza mapokezi ya mtambo wa megawati 20 utakaozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia. 

Muonekano wa mtambo wa kuzalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia wa Megawati 20 unaotumia injini ya ndege aina ya Boeing 747 ambao umeletwa nchini kwa ajili ya kutatua changamoto ya Umeme mkoani Lindi na Mtwara.

Mtambo huo aina ya TM16 wenye mfano wa injini ya ndege ya Boeing 747 utafungwa katika  Kijiji cha Hiari, Wilaya ya Mtwara Vijijini ikiwa ni maelekezo ya Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Wizara ya Nishati kuhakikisha kuwa changamoto ya upatikanaji umeme kwenye mikoa hiyo inatatuliwa. 

Akipokea mtambo huo kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhe. Felchesmi Mramba, amesema kuwa mtambo huo utaondoa changamoto ya upatikanaji wa umeme kwenye Mkoa wa Lindi na Mtwara. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba akipokea mtambo wa kuzalisha umeme wa Megawati 20 kwa ajili ya kutatua changamoto ya umeme kwa mikoa ya Lindi na Mtwara. Amepokea mtambo huo wilayani Mtwara tarehe 09 Februari, 2024.

“Mhe. Rais alitoa maelekezo kwa Wizara ya Nishati, kufanya kila jitihada ili changamoto ya umeme kwenye mikoa hiyo itatuliwe kwa haraka, tunashukuru leo tumeweza kutimiza ahadi hiyo  kwani mtambo huu ni miongoni mwa mitambo ya kisasa kabisa ya umeme iliyowahi kuletwa nchini ambayo inatoa uhakika wa kuzalisha umeme kwa kipindi kirefu.” Amesema Mha.Mramba 

Aidha, Mhandisi Mramba ameongeza kuwa, maelekezo Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati kuhusu kuepeleka umeme wa gridi kwenye mikoa hiyo yameshaanza kutekelezwa ambapo kabla ya mwezi wa sita mwakani umeme wa Gridi ya Taifa utakuwa umefika kwenye mikoa ya Lindi na Mtwara. 

Kuhusu maelekezo aliyoyatoa Naibu Waziri Mkuu na  Waziri wa Nishati ya kuhakikisha wananchi  wa mikoa hiyo inayozalisha gesi kwa wingi wananufaika na uwepo wa nishati hiyo, amesema tayari wameanza kuboreshewa huduma mbalimbali ikiwemo kuwajengea kituo cha Polisi, ununuzi wa boti ya kisasa kwa ajili ya usafiri wa wananchi eneo la Songosongo mkoani Lindi na ujenzi wa kituo cha afya eneo la Madimba mkoani Mtwara.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Ahmed Abbas Ahmed alisema kuwa, wananchi wa Mtwara wamepokea kwa furaha mtambo huo ambao utafungua fursa za uwekezaji kwa kutokana na kuwepo kwa umeme wa uhakika  kwani takriban asilimia 80 ya matumizi ya umeme mkoani humo yanatumika kwenye sekta ya biashara. 

“Tunamshukuru sana Mhe. Rais, Dkt. Samia kwa kutimiza ahadi yake na na mapenzi ya dhati aliyoyaonyesha kwa wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara na kufanya mikoa hii kupata umeme wa uhakika ambao utainua sekta ya uchumi kwa ujumla.” Amesema Kanali Ahmed 

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Kilumbe Ng’enda ameishukuru Serikali kupitia Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati  Mhe. Dkt.  Doto Biteko kwa kusikiliza kilio cha wabunge wa mikoa juu ya changamoto ya upatikanaji wa umeme wa uhakika  na kuipongeza Wizara ya Nishati kwa hatua kubwa inazochukua  kuhakikisha sekta ya umeme inaimarika.

Post a Comment

Previous Post Next Post