YOUR FUTURE IS CREATED BY WHAT YOU DO TODAY, NEVER TOMORROW

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  George Simbachawene amesema Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) tangu kuanzishwa kwake katika Usharika wa Kibakwe limekuwa neema na baraka kubwa kwa wakazi wa eneo hilo huku akisema limeleta mapinduzi makubwa kiuchumi na kifikra kwa wananchi.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  George Simbachawene

Waziri Simbachawene ameyasema hayo leo Jumapili Juni 16, 2023 alipokuwa akizungumza na Viongozi wa Dini na Washarika katika Ibada Takatifu ya kumwingiza kazini Mkuu wa Jimbo la Kibakwe, Dayosisi ya Dodoma ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mchungaji Emanuel Milangasi iliyoongozwa na Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Dodoma, Christian Ndossa katika usharika wa Kibakwe, Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa jijini Dodoma.

 

Amesema Kanisa hilo limekuwa chachu kwa Wakazi wa Kibakwe na wengine katika suala zima la maendeleo na hivyo kumpelekea yeye kama Mbunge wa Jimbo hilo na Waziri anayeshughulikia masuala ya utawala bora kupata urahisi pindi anapohamasisha masuala ya maendeleo.

 

Akitolea mfano kuwa tangu kuanzishwa kwa Kanisa hilo limekuwa mstari wa mbele katika kutoa huduma za kiroho na kijamii kwa Washarika hao.

 

Aidha, Simbachawene amesema Kanisa hilo limeleta umoja na mshikamo katika jamii kupitia mafundisho yake ambayo yamejikita kwenye kuhubiri upendo.

 

"Ukizungumzia maendeleo ya Jimbo la Kibakwe huwezi kuacha kulitaja Kanisa la KKKT la Usharika wa Kibakwe" amesema Simbachawene.


 

Amefafanua kuwa Kanisa hilo limeleta mageuzi makubwa katika Jimbo hilo ikiwa ni pamoja  na kuwa wamiliki wa mwanzo kabisa wa Nyumba ya kulala na kutumia nishati ya jua kwa ajili ya kusambaza huduma ya maji kwa wananchi.

 

Kufuatia hatua hiyo, Mhe. Simbachawene ameliomba Kanisa hilo kuendelea kuwekeza zaidi katika kutoa huduma za jamii ikiwemo ujenzi wa kituo cha watoto yatima pamoja na shule.

 

Aidha, Simbachwene ametumia fursa hiyo kumhakikishia Mkuu huyo mpya wa Jimbo, Mchungaji Emanuel Milangasi kuwa atampa ushikirikiano kwa lengo la kuijenga Kibwake mpya yenye hofu ya Mungu na yenye uchumi endelevu.

 

Hata hivyo Simbachawene amewasihi Washarika hao kumpa ushikiano Mchungaji huyo ili aweze kutekeleza majukumu yake ya kutoa huduma ya kiroho kwa Washarika kama ilivyokusudiwa.   

 

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Dodoma KKKT, Christian Ndossa amemshukuru Waziri Simbachawene kwa kukubali kushiriki katika Ibada hiyo Takatifu katika Usharika wa Kibakwe huku akimhakikishia kuwa watazidi kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kuendelea kutekeleza majukumu yake mazito aliyo nayo kwa maslahi mapana ya kitaifa.

 

Pia, Askofu Christian Ndossa amemtakia majukumu mema katika kumsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kufikia malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwaletea maendeleo Watanzania.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post