Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kukamata simu 61 kutoka kwa wanawake watatu wanaofanya shughuli za wizi kwenye maeneo ya minada na hukwapua mali hizo wanapolala na wanaume.


Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari Disemba 20, 2023 Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi amesema simu hizo na watuhumiwa watatu wamekamatwa katika misako inayofanywa na jeshi la polisi kwa lengo la kuimarisha Usalama wa Raia na Mali zao hasa katika kipindi hiki kuelekea Sikukuu za Chrismas na Mwaka mpya ili kuhakikisha wananchi wa Mkoa wa Shinyanga wanasherekea Sikukuu hizo kwa amani na utulivu.

"Tunawashikilia wanawake watatu raia wa Burundi ambao wameingia nchini kwa njia haramu na wamekuwa wakifanya wizi, tumewakamata wakiwa na simu 61 walizoiba kwenye minada ya Kahama, Mwanza na Shinyanga. Lakini akina dada hawa pindi wanapolala na wanaume huwaibia na kuwatoroka wanaume hao",amesema Kamanda Magomi.

 
"Kufuatia Doria na misako hiyo iliyofanyika katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Shinyanga, Mwezi Novemba 30, 2023 hadi Disemba 19, 2023 Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kukamata Simu 61 ambazo zimekamatwa kutoka wa akina dada waliokuwa wanafanya shughuli za wizi, pombe ya moshi Lita 173, mafuta ya dizeli Lita 260, Pikipiki 07, TV 04, vyuma vya kuchimbia visima 09, Goroli za Karasha 106, Bangi misokoto 15, Subwoofer 02, Difu 01 ya Gari aina ya Toyota Hiace pamoja na noti bandia 09 zenye thamani ya Tshs.85,000/=",ameeleza Kamanda Magomi.

Amevitaja vitu vingine vilivyokamatwa ni pamoja na Pipe 11 za kunyonya mafuta, Baiskeli 01, vipande vya nondo 06, Keyboard 01, Chesess 01 ya Pikipiki, Spika 02, na vifaa mbalimbali vya kupigia ramli chonganishi ambavyo ni mikia 08 idhaniwayo kuwa ni ya mnyama aina ya Nyumbu, kipande 01 cha Ngozi ya Simba. 

 
Katika upande wa mafanikio ya kesi Mahakamani, Kamanda Magomi amesema jumla ya kesi 08 zilipata mafanikio ambapo kesi 01 ya kubaka mshitakiwa alihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela, kesi 02 za kujipatia pesa kwa njia ya udanganyifu washitakiwa walihukumiwa kwenda jela kati ya miezi 06 hadi miaka 03.

"Nyingine ni kesi 01 ya kuharibu mali mshitakiwa alihukumiwa kwenda jela miezi 05, kesi 02 za wizi wa pikipiki washitakiwa walihukumiwa kwenda jela kati ya miaka 02 hadi 03, kesi 01 ya kupatikana na mali idhaniwayo kuwa ya wizi mshitakiwa alihukumiwa kwenda jela mwaka 01, Kesi 01 ya wizi wa kuaminiwa washitakiwa 06 walihukumiwa kutotenda kosa lolote kwa mwaka 01. Kesi 01 ya kutishia kuua kwa Silaha panga mshitakiwa alihukumiwa kutotenda kosa lolote kwa mwaka 01",ameongeza.

Aidha katika kudhibiti ajali za Usalama Barabarani Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kukamata jumla ya makosa mbalimbali 2806, kati ya hayo makosa 05 yalikamatwa kwa kusababisha ajali, kuendesha mwendokasi na matumizi mabaya ya barabara na madereva kulipa faini.

"Pamoja na hatua mbalikmbali tunazoendelea kuzichukua katika kudhibiti ajali za barabarani pia Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Shinyanga kimefanikiwa kutoa elimu kwa makundi yote yanayotumia barabara kwa lengo la kupunguza ajali za barabarani na linawasisitiza madereva kufuata sheria wenyewe bila kusimamiwa na askari, dereva yeyote atakayevunja sheria atashughulikiwa kwa mujibu wa sheria",amesema.

Post a Comment

Previous Post Next Post