YOUR FUTURE IS CREATED BY WHAT YOU DO TODAY, NEVER TOMORROW

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amekutana na kufanya mazungumzo na watendaji wa Kampuni ya Mufindi Paper Mill inayomiliki mashamba ya miwa wilayani Kasulu mkoani Kigoma ambao wamweleza Naibu Waziri wa Nishati, kuhusu nia yao ya kuzalisha umeme kwa kutumia mabaki ya miwa ifikapo mwaka 2026.

 

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga akizungumza na Ujumbe wa Kampuni ya Mufindi Paper Mill inayotarajia kuzalisha Umeme wa Megawati 24 kwa kutumia mabaki ya Miwa katika Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma, (hawapo pichani) waliofika kujitambulisha kwa Naibu Waziri huyo na kumueleza mipango ya uwekezaji wa kampuni hiyo, tarehe 6 Novemba 2023, Jijini Dodoma.
 

Na Mwandishi Wetu.

 

Kikao hicho kimefanyika Jijini Dodoma tarehe 6 Novemba, 2023 na kuhudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Isaac Mwakisu, Watendaji kutoka Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

 

Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Anoop Singh amemweleza Naibu Waziri kuwa, kampuni hiyo ambayo ina hekta za 30,000 za mashamba ya miwa wilayani Kasulu mkoani Kigoma mwaka 2026 inatarajia kuzalisha umeme wa kiasi cha Megawati 24 na ifikapo mwaka 2028 wataongeza uzalishaji na kufikia Megawati 60.

 

Wataalamu kutoka Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Ujumbe kutoka Kampuni ya Mufindi Paper Mill inayotarajia kuzalisha Umeme wa Megawati 24 kwa kutumia mabaki ya Miwa katika Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma,wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati, Judith wakati wa Kikao na Ujumbe huo, tarehe 6 Novemba 2023, Jijini Dodoma.


Ujumbe wa Kampuni ya Mufindi Paper Mill inayotarajia kuzalisha Umeme wa Megawati 24 kwa kutumia mabaki ya Miwa katika Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma, wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga (hayupo pichani) walipofika kujitambulisha kwa Naibu Waziri huyo na kumueleza mipango ya uwekezaji ya Kampuni yao, tarehe 6 Novemba 2023, Jijini Dodoma. 

 

Amesema kuwa, umeme utakaozalishwa na kampuni hiyo utatumika kuendeshea mitambo katika kampuni hiyo na mwingine wanatarajia kuingizwa katika gridi ya Taifa baada ya majadiliano na TANESCO.

 

Ili kuweza kufanikisha nia hiyo ya kuzalisha umeme, Sigh alimweleza Naibu Waziri kuhusu maombi mbalimbali ikiwemo ya kujengewa miundombinu ya kusafirisha umeme ya kV 132 au 400 kV kutoka kwenye kiwanda ili kuingiza umeme kwenye gridi ya Taifa na kujengewa kituo cha umeme cha kV 11/132 kV au kituo cha 11kV/400kV.

 

Naibu Waziri wa Nishati, ameipongeza kampuni hiyo kwa uwekezaji huo na kueleza kuwa Serikali itaendelea kuwapa ushirikiano kadri itakavyowezekana kwani nia ya Serikali ni kufanya kazi pamoja na Sekta Binafsi katika nyanja mbalimbali ikiwemo umeme.

 

Kuhusu maombi mbalimbali yaliyowasilishwa na kampuni hiyo, Naibu Waziri ameelekeza wataalam kutoka TANESCO kushirikiana na Wataalam kutoka kampuni hiyo ili kuona namna bora ambayo Serikali kupitia TANESCO inaweza kutekeleza maombi hayo.

 

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Nishati amefanya mazungumzo na watendaji kutoka Kampuni ya Songas wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Anael Samuel ambaye alieleza nia yao ya kujitambulisha kwa Naibu Waziri pamoja na kumweleza taarifa za sasa kuhusu uendeshaji wa kampuni hiyo inayozalisha umeme wa Megawati 190 na kuingiza katika gridi ya Taifa.

 

 

Post a Comment

Previous Post Next Post